Chumvi inapotumika kwa kiasi kidogo haina madhara. Miili yetu inahitaji chumvi kwa kiasi kidogo sana kwasababu chumvi huupatia mwili madini ya Sodium yanayohitajika kusafirisha taarifa za mfumo wa fahamu, kudhibiti kiwango cha maji katika damu, ukunjikaji au kujivuta kwa misuli, udhibiti wa kiwango sahihi cha maji na uwiano sahihi wa chumvichumvi mwilini.
Mwili unapata pia madini haya kutoka kwenye vyakula vingine kama maziwa na mayai, hivyo chumvi itumike kwa kiasi kidogo tu.
Chumvi yote inayotumika inapaswa kuwa na Lodone ambayo ni muhimu kwa ubongo wenye afya kwa mtoto aliye tumboni na anayekuwa pia huimarisha utendaji wa ubongo kiujumla. Matumizi makubwa ya chumvi ya zaidi ya gramu (2-5) kwa siku, huchangia kupanda kwa shinikizo la damu na kuongezeka hatari ya kupata ugonjwa wa moyo na kiharusi.
Watu wengi hutumia chumvi nyingi kwenye vyakula vyao, kwa wastani wengi hutumia gramu (9-12) kwa siku au mara mbili ya kiwango kinachopendekezwa.
Matumizi makubwa ya chumvi yana madhara gani?
Matumizi ya chumvi nyingi yanaongeza uwezekano wa kupata shinikizo kubwa la damu, kwani chumvi husababisha maji kujikusanya mwilini. Maji yaliyojikusanya huongeza shinikizo kwenye moyo na mishipa ya damu na hivyo kusababisha moyo kufanya kazi kwa nguvu zaidi.
Shinikizo kubwa la damu huongeza uwezekano wa kupata magonjwa mengine sugu kama yale ya figo, moyo na pia mifupa kama "Osteoporosis". Hivi karibuni tafiti zimeonyesha uhusiano mkubwa kati ya matumizi ya vyakula vilivyosindikwa au kuhifadhiwa kwa chumvi na saratani ya tumbo.
Mapendekezo ya kutumia chumvi kulingana na rika
Watu wazima, Shirika la Afya Duniani (WHO) linashauri watumie chumvi chini ya gramu 5 (Chumvi isiyozidi kijiko cha chai) kwa kila siku nzima.
Watoto (Miaka 2-15), Shirika la Afya Duniani (WHO) linashauri watumie chumvi chini ya kiwango cha juu cha matumizi ya chumvi kwa wakubwa kwa kuwa mahitaji ya nishati kwa mtoto na mkubwa hutofautiana.
Je, nini kifanyike ili kupunguza matumizi ya chumvi?
Nchi wanachama wa Shirika la Afya Duniani (WHO) zimekubali kupunguza matumizi ya chumvi kwa angalau asilimia 30 kufikia 2025.
Kupunguza matumizi ya chumvi hupunguza gharama kwa nchi kuboresha afya za wananchi wake. Inakadiriwa vifo milioni 2.5 vingeweza kuzuiwa kila mwaka endapo matumizi ya chumvi duniani yangepunguzwa kufikia kiwango kinachokubalika.
Jinsi ya Kupunguza Matumizi ya Chumvi, ngazi ya Taifa
Kutokana na hali kuwa hatari zaidi naishauri Serikali iweze kuunda sera zitakazowabana wazalishaji na wauzaji wa vyakula, kutengeneza vyakula vyenye ubora kiafya na vya gharama nafuu. Aidha, iweze kudhibiti na kufuatilia matumizi ya chumvi kwenye jamii, kujua vyanzo vya chumvi na uelewa wa watu kuhusu matumizi ya chumvi.
Pia pamoja na hayo inatakiwa iweka mazingira mazuri ya kupunguza matumizi ya chumvi kwa kutekeleza sera na kuhamasisha vyakula vyenye afya sehemu kama shuleni, vyuoni n.k,Kufanya kazi na sekta binafsi kuboresha upatikanaji wa vyakula vyenye chumvi kidogo.
Kama mtaalam wa afya nawashauri wasomaji wa FikraPevu na Serikali kwa ujumla kupitia wizara zinazohusika waweze kuwapa elimu, utumiaji kwa vikundi juu ya umuhimu wa kupunguza matumizi ya chumvi.
Jinsi ya Kupunguza Matumizi ya Chumvi, ngazi ya mitaa
Kujumlisha elimu ya kupunguza matumizi ya chumvi kwenye mafunzo ya waandaaji vyakula hasa mama lishe. Kuondoa mikebe ya chumvi kwenye meza za migahawa pamoja na kuweka lebo kwenye bidhaa zenye Sodium/chumvi nyingi.
Kutoa elimu ya lishe bora ukilenga matumizi ya chumvi kwa wateja/wagonjwa waliohudhulia vituo vya kutolea huduma za afya.
Kuelimisha watoto na kuwapa ushirikiano ili kuwazoeza kutumia kiwango kidogo cha chumvi kwenye vyakula vyao tangu wakiwa watoto.
Jinsi ya Kupunguza Matumizi ya Chumvi, ngazi ya familia
(i) Punguza chumvi inayowekwa kwenye chakula wakati wa kuandaa au kupika chakula, kudhibiti matumizi ya vitafunwa vyenye chumvi mfano chips.
(ii) Usiweke chumvi mezani, kwa kuwa mara nyingi watu huongeza chumvi bila hata kuonja.
(ii) Epuka vyakula vilivyosindikwa kwa kutumia au kuongezwa chumvi, kama nguru aliyekaushwa kwa chumvi, baadhi ya vyakula vya makopo au paketi.
(iv) Ni vyema kusoma lebo kwa makini na chagua vyakula vilivyosindikwa bila ya chumvi iliyoongezwa (No salt added) au chagua bidhaa zenye sodium ndogo ndani yake.
(v) Tumia zaidi vyakula fresh unavyopika mwenyewe kwani unaweza kudhibiti kiasi cha chumvi unachotumia.
(vi) Tumia zaidi viungo kuongeza ladha kwenye chakula, mfano vitunguu saumu, tangawizi n.k
Maswali yaulizwayo mara kwa mara kuhusu chumvi
Swali: Je, unahitaji chumvi nyingi kwenye chakula ili kurudishia chumvi mwilini iliyopotea wakati unatokwa jasho jingi kipindi cha jua na joto kali?
Jibu: Hapana, hauhitaji kula chumvi nyingi kwa kuwa ni kiwango kidogo sana cha chumvi hupotea kwa njia ya jasho ingawa ni muhimu kunywa maji kwa wingi.
Swali: Je, chumvi ya baharini ni bora zaidi kuliko ya kiwandani kwa kuwa ni ya asili?
Jibu Hapana, bila kujali chanzo cha chumvi ni Sodium ile ile iliyomo kwenye chumvi ambayo husababisha matatizo ya kiafya.
Swali: Je, chumvi inayoongezwa wakati wa kupika sio chanzo kikuu cha chumvi inayotakiwa mwilini?
Jibu: Hapana, katika nchi nyingi asilimia 80 ya chumvi kwenye vyakula hupatikana kwenye vyakula vilivyosindikwa viwandani.
Swali: Je, chakula hakina ladha bila chumvi nyingi?
Jibu: Hapana, ingawa inaweza kuwa kweli mwanzoni ambapo vionja ladha vinakuwa havijazoea chumvi kidogo ila muda unavyozidi kwenda unazoea na kufurahia ladha ya chakula kama kawaida.
Swali: Je, ni kweli vyakula vyenye chumvi nyingi vinakuwa na ladha ya chumvichumvi?
Jibu: Hapana, kwa kuwa baadhi ya vyakula vyenye chumvi nyingi wakati mwingine huchanganywa na vitu vingine kama sukari na kufanya viwe na ladha isiyo na chumvi nyingi.
Swali: Je, ni watu wenye umri mkubwa tu ambao wanapaswa kuhofia juu ya matumizi makubwa ya chumvi?
Jibu: Hapana, ulaji wa chumvi nyingi unaweza kusababisha kupanda kwa shinikizo la damu katika umri wowote.
Swali: Je, kupunguza chumvi kunaweza kuwa ni hatari kwa afya yako?
Jibu: Hapana, kwa kuwa ni vigumu sana kula chumvi chini ya kiwango wakati kuna vyakula vingi vilivyo na chumvi tunavyokula kila siku mfano maziwa na mayai.
The post Jinsi ya Kupunguza Matumizi ya Chumvi katika Ulaji wa Vyakula na mengineyo appeared first on Fikra Pevu.