KATIKA siku za hivi karibuni, dunia imekuwa ikihamasisha jamii zote kutambua madhara ya tumbaku kwa afya ya binadamu na hata katika uharibifu wa mazingira. Taarifa zinasema kwamba serikali inatumia mabilioni ya shilingi kila mwaka kutibu wagonjwa wanaotokana na uvutaji wa tumbaku na wengine kupoteza maisha huku wengi wao wakiwa ni maskini.
Matumizi ya tumbaku yamethibitika kisayansi kudhuru karibu viungo vyote vya mwilini na kusababisha magonjwa kama vile saratani na kifo. Mbali ya kuwa ina madhara kiafya, tumbaku inasababisha uharibifu wa hekta takribani 1200 za misitu zinamalizwa kila mwaka kutokana na ukataji wa miti kwa ajili ya kuni za kukaushia tumbaku.
Mataifa mengi yamefanya jitihada nyingi ili kupambana na janga hili la kiafya, mazingira na uchumi. Kufikia Agosti, 2012 nchi 175 zilikubaliana kuchukua hatua kukomesha matumizi ya tumbaku. Hata hivyo, kuna mambo yanayoendeleza zoezi hilo.
Kila mwaka, kampuni za kutengeneza tumbaku hutumia pesa nyingi katika matangazo ya kibiashara ili kuvutia wateja wapya, hasa wanawake na vijana katika nchi zinazoendelea.
Kwanini ni vigumu kuacha kuvuta tumbaku?
(i) Vitu vinavyotengenezwa kutokana na tumbaku vinaweza kumfanya mtu awe mraibu (Addicted) kama ilivyo kutumia dawa za kulevya.
(ii) Mtu anapovuta nikotini, inaingia ndani ya ubongo baada ya sekunde saba tu. Nikotini ina asili ya sumu isiyoachika ndani yake.
(iii) Mara nyingi kuvuta tumbaku huwa ni sehemu muhimu ya maisha ya mtu kwa kuwa anaivuta anapokula, anapokunywa, anapozungumza, anapotaka kuondoa mfadhaiko na kadhalika.
(iv) Wavutaji hawajajikubalisha kwamba sigara ni haramu na sio nzuri kiujumla.
Jinsi ya kuacha kuvuta tumbaku
Andika sababu kwanini unataka kuacha kuvuta sigara, Maandishi hayo unapaswa kuwa nayo karibu ili iwe vyepesi kuangalia pale unaposhawishika kuvuta sigara, panga tarehe mahususi ya kuacha kuvuta na uache mara moja tarehe ikifika.
Baadhi ya wataalamu hushauri kuacha taratibu ingawa utafiti unaonyesha kwamba endapo mvutaji atavuta sigara chache tofauti na mwanzo basi kuna uwezekano wa kuvuta mpaka mwisho kila moja ya sigara hizo, hali hii hupelekea kiwango cha nikotini kuwa juu karibu na ilivyokuwa mwanzo. Hivyo ni bora zaidi kuacha mara moja ikifika tarehe iliyopangwa.
Imarisha azimio lako
Ukitaka kuacha kuvuta sigara unapaswa kuazimia kabisa kuacha. Fikiria jinsi utakavyo faidika ukiaacha kuvuta sigara ikiwa ni pamoja na kuokoa pesa, afya yako inaweza kuwa nzuri zaidi, utampendeza Muumba wako n.k
Tafuta msaada na mwambie azimio lako.
Watafute wale ambao wamefaulu kuacha zoea hilo kwa kuwa huenda zaidi ya kuelewa hisia zako, wanaweza kukusaidia. Marafiki na washiriki wa familia mara nyingi hutoa ushirikiano kwako ili uweze kutimiza azma yako.
Kama kuna wenzako unaoishi nao wanavuta tumbaku washawishi waache pamoja nawe kwa kuwa nguvu za pamoja ni tofauti na nguvu ya mmoja kupambana na tatizo hili. Usipowashawishi kuacha wanaweza kukushawishi kurudia tabia yako ya uvutaji tumbaku hata kama uliazimia kuacha.
Teketeza vitu vyote vinavyokufanya uvute Tumbaku mfano kiberiti cha kuwashia tumbaku, jiandae kukabiliana na madhara yatokanayo na kuacha kuvuta tumbaku.
Uchunguzi wa wataalamu wetu wa FikraPevu unaonyesha kwamba karibu asilimia 90 ya wale wanaojikwaa hurudia zoea lao. Unapoacha kuvuta unaweza kupatwa na dalili za ajabu mfano hamu ya kutumia nikotini, kichefuchefu, kujisikia mgonjwa, kichwa kuuma, kushuka moyo, kutokuwa na subra na kujisikia vibaya tu.
Dalili hizi hutokea kutokana na mwili kukosa nikotini iliyokuwa ya kawaida mwilini. Dalili hizi hupamba moto masaa 12 hadi 24 baada ya kuacha kuvuta tumbaku na taratibu huacha kati ya wiki ya pili hadi sita.
Mambo yanayoweza kukusaidia ni pamoja na kulala kwa muda mrefu zaidi, kunywa maji mengi au maji ya matunda, kula chakula chenye lishe, kufanya mazoezi ya kadiri na kuvuta pumzi kabisa na uwazie hewa safi ikijaa ndani ya mapafu yako.
Tegemea kupatwa na kikohozi
Ni kawaida kupatwa na kikohozi pale unapoacha kuvuta tumbaku kwasababu njia za hewa zinaanza kurudi katika uhai wake. Watu wengi hudai kikohozi hufanya hali kuwa mbaya na kuwashawishi kurudia kuvuta tumbaku. Jitahidi kujizuia kwa kuwa kikohozi hiki hupotea chenyewe jinsi muda unavyopita.
Zitambue hali zote zinazopelekea utake kuvuta.
Mara nyingi unywaji wa pombe huzuia jitihada za kuacha kuvuta tumbaku. Unapaswa kupunguza sana kiwango cha pombe utakachokunywa pale utakapoacha kuvuta sigara endapo utashindwa kuacha kabisa. Pia unashauriwa kunywa maji mengi na maji ya matunda.
Zikumbuke siku zote unazofanikiwa kutovuta tumbaku
Weka alama kwenye kalenda kwa siku zote unazofanikiwa kuacha kuvuta na ziangalie pale unaposhawishika kuvuta, huku ukijiambia sipaswi kuanza tena upya.
Kuwa mwenye mawazo chanya
Unaweza kuwaambia wengine huvuti, utakuwa na harufu nzuri. Baada ya wiki chache utajisikia vizuri zaidi, utapata ladha nzuri ya vyakula na hutokohoa. Pia utakuwa na hela zaidi kwa kuwa hukutumia kununua tumbaku.
Vyakula vinavyotakiwa kwa wanaojaribu kuacha kuvuta.
Watu wengine huwa na hofu ya kunenepa wakiacha kuvuta sigara kwa kuwa hamu na ladha ya vyakula huwa bora zaidi pindi wanapoacha kuvuta tumbaku. Yapaswa utegemee kuongezeka kwa ladha na hamu ya vyakula ila jitahidi kutokula vyakula vya wanga na mafuta kwa wingi badala yake ule vyakula vingine na matunda.
Usikate tamaa pale unaposhindwa.
Chunguza ni kwanini ulishindwa wakati uliopita na jirekebishe. Kwa wastani watu waliofanikiwa kuacha kuvuta wamewahi kujaribu kuacha mara 3 hadi 4 wakati uliopita.
Tembelea kliniki za kuzuia uvutaji.
Madaktari wanaweza kukupa msaada unaouhitaji endapo unafikiri ni vigumu kuacha kuvuta tumbaku, madawa mbalimbali yanaweza kukusaidia kuacha kuvuta tumbaku.
Katika uchunguzi mmoja, asilimia 88 ya watu waliofaulu kuacha kuvuta sigara walisema walifanya hivyo bila kutumia dawa zozote. Madawa haya huhusisha madawa mbadala ya nikotini na huwa katika mifumo tofauti kama vidonge na chingamu. Pia kuna sigara za kieletroniki (E-cigarette) ambazo zimetengenezwa na hukufanya ujisikie kama unavuta sigara ya kawaida.
Uwe mteuzi wa marafiki
Epuka kuwa na watu wanaovuta tumbaku wanaoweza kukupa sigara. Pia, waepuke watu wanaojaribu kuvuruga jitihada zako za kuacha kuvuta tumbaku, labda kwa kukudhihaki.
Dhibiti hisia zako
Katika uchunguzi mmoja karibu asilimia 66 ya wale walio anza tena kuvuta sigara walifanya hivyo baada tu ya kufadhaika au kupandwa na hasira. Ukipatwa na hisia fulani inayokuchochea kuvuta sigara, jikengeushe fikra labda kwa kunywa maji, kutafuna chingamu au kutembea.
Jaribu kufikiria mambo yanayofaa
Mtegemee muumba wako ukiwa na azma ya moja kwa moja kutorudia kuvuta tumbaku, kwa kuridhia amri zake.
Visingizio unavyopaswa kuepuka.
(i) Ninavuta mara moja tu. Ukweli ni kwamba kuvuta mara moja tu kunaweza kutosheleza asilimia 50 hivi ya vipokezi vya nikotini kwenye ubongo kwa saa tatu. Matokeo yatakuwa kwamba utaanza tena kuvuta sigara.
(ii) Kuvuta sigara hunisaidia kutuliza mfadhaiko. Uchunguzi wa FikraPevu unaonyesha kwamba nikotini huongeza kiwango cha homoni zinazomfanya mtu afadhaike. Hisia zozote zinazokudanganya kuwa mfadhaiko wako hupungua unapovuta sigara zinaweza kuwa zinasababishwa tu na athari za kuacha kuvuta sigara.
(iii) Nimekuwa nikivuta sigara kwa muda mrefu sana siwezi kuacha, hivyo usifikirie huwezi kuacha kuvuta sigara.
(iv) Siwezi kukabiliana na athari zinazosababishwa na kuacha kuvuta sigara. Ni kweli kwamba athari za kuacha kuvuta sigara zina nguvu, lakini zitapungua baada ya majuma machache tu.
(v) Nina tatizo la akili. Ikiwa unatibiwa tatizo lako la akili, kama vile mshuko wa moyo au schizophrenia, mwombe daktari akusaidie uache kuvuta sigara. Bila shaka atajitahidi kukusaidia labda hata atabadili matibabu yako ili yasiongeze ugonjwa wako au kuathiri dawa unazotumia.
Faida za kuacha kuvuta tumbaku
Utafurahia maisha zaidi. Watu wanapoacha kuvuta tumbaku, uwezo wao wa kunusa na kuonja unaboreka na kwa kawaida wana kuwa na nguvu zaidi na sura yao inapendeza zaidi. Utaokoa pesa, afya yako inaweza kuwa nzuri zaidi, Utajiamini zaidi, familia yako na marafiki watafaidika, utampendeza muumba wako.
The post Madhara ya Matumizi ya bidhaa za Tumbaku Kiafya na Kijamii appeared first on Fikra Pevu.